Tip:
Highlight text to annotate it
X
"Siku yake Imemalizika" Shairi la wasifu wa Nelson Mandela
lililotungwa na Maya Angelou kwa niaba ya raia wa Marekani.
Siku yake imemalizika.
Imemalizika.
Habari zilivuma kwenye bawa za upepo
zikisita kubeba mzigo wake.
Siku ya Nelson Mandela imemalizika.
Habari, zisizotarajiwa na bado zisizokaribishwa
sisi Marekani
kwa ghafla zimetufika ulimwengu wetu majonzi ukajaa.
Mawingu yetu yakatanda,
siku yake imemalizika.
Twawaona, watu wa Afrika kusini wakisimama
kwa kubutwaika baada ya lango hilo kufungwa
na kuhitimika ambalo msafiri akipita hapati kurejea.
Roho zetu zaja kwenu Wabantu, Wazulu, Waxhosa, Makaburu.
Tunawaweka kwenye fikra zetu na mwana wenu wa Afrika,
baba yenu, moja kati ya maajabu ya dunia aliyekuwa mwenzenu.
Mioyo yetu yaja
kwenu mnapotafakari juu ya Daudi
aliyekuwa wenu na jiwe moja
tu akipambana na Goliathi mkubwa sana
Gidioni mwenye nguvu sana, akiibuka mshindi.
Ingawa kazaliwa katika enzi katili za kibaguzi.
Akiwa na makovu ya ubaguzi wa rangi,
kafungwa jela bila kisa katika mapango
ya Afrika kusini yenye damu.
Angesalimika mtu huyu? Angeweza kusalimika?
Majibu yake yalituimarisha sote
wanaume kwa wanawake duniani kote.
Katika Alamo mjini San Antonio, Texas
katika daraja kuu la Golden Gate mjini San Francisco,
katika jiji la Chicago,
Kwenye Mardi Gras ya New Orleans,
katika Times Square ya New York,
Tulitazama pale matumaini ya Afrika
yalipoibuka kwenye milango ya jela
Moyo wake wa kijasiri ukiwa imara,
ya dhati yake nia mwenye ari na bashasha.
Ukatili haukumlemaza juu ya imani
yake na hisia za haki za binadamu hazikuzimwa
maji na kifungo cha miaka ishirini na saba.
Hata hapa Marekani
tulipulizwa na upepo muruwa wa uhuru.
Nelson Mandela alipochukua kiti cha urais nchini mwake
ambapo awali hakuruhusiwa hata kupiga kura.
Kwa machozi ya fahari tulitanuka tuliposhuhudia walinzi
wa zamani jela wa Nelson Mandela wakikaribishwa,
kwa ukarimnu, kushuhudia mbele kwenye jukwaa kutawazwa kwake.
Tulimwona akipokea tuzo ya dunia nchini Norway
kwa neema na shukrani kama
wahenga wa mahakama za kale za Warumi.
Na uhakika wa Watemi wa Kiafrika kwenye viti vyao vya kale.
Hakuna jua linalodumu kwenye machweo
lakini kutakucha tena na kuleta alfajiri.
Ndiyo, siku ya Mandela imemalizika,
lakini sisi, warithi wake,
tutafungua milango ya mapatano
na tutaitikia kwa ukarimu
kwa vilio vya Weusi na Weupe,
Waasia na Wahispenia,
mafukara wanaoishi kwa huruma kwenye sakafu ya sayari yetu.
Ametupa uelewano,
tusiwe wachoyo wa msamaha
hata kwa wale ambao hawajaomba.
Siku ya Mandela imemalizika,
tunakiri kwa sauti za vilio
bali tunanyanyua sauti zetu kusema asante.
Asante, Gidioni wetu,
asante Daudi wetu,
mtu wetu mwenye ujasiri mkubwa.
Katu hatutakusahau,
katu hatutashusha hadhi yako,
Tutakumbuka na kufurahi kwamba
uliishi miongoni mwetu
kwamba ulitufundisha
na kwamba ulitupenda sote!
"Siku yake Imemalizika" Shairi la wasifu wa Nelson Mandela
lililotungwa na Maya Angelou kwa niaba ya raia wa Marekani